Sunday 19 May 2013

Korea Kaskazini yarusha makombora ya masafa mafupi

Raia mmoja wa Korea Kusini akifuatilia kwenye televisheni urushaji wa makombora uliofanywa na Korea Kaskazini.Raia mmoja wa Korea Kusini akifuatilia kwenye televisheni urushaji wa makombora uliofanywa na Korea Kaskazini.
ukubwa wa habari
Korea Kusini inasema Korea Kaskazini imefyatua makombora matatu ya masafa mafupi katika bahari ya East Sea ambayo pia hujulikana kama Sea of Japan.

Wizara ya Ulinzi ya Korea Kusini inasema imegundua kurushwa kwa makombora mawili Jumamosi asubuhi, na jingine lilirushwa nyakati za mchana.

Msemaji wa wizara hiyo, Kim Min-seok anasema azma ya Kaskazini haiko bayana. Anasema jeshi la Korea Kusini linafuatilia kwa karibu urushaji mwingine wowote na uwezekano wa uchokozi.

Shirika la habari la Japan, Kyodo limeripoti kuwa afisa mmoja wa Japan amethibitisha kuhusu majaribio hayo na kusema makombora hayakuangukia katika maji ya Japan.

Maendeleo haya yamekuja katika kipindi cha mawasiliano ya kidiplomasia yanayolenga kupunguza mivutano. Mapema mwaka huu, Pyongyang ilitishia kufanya mashambulizi ya nyuklia kwa Korea Kusini na Marekani kufuatia  mazoezi ya kijeshi ya kila mwaka kati ya Marekani na Korea Kusini na vikwazo vya Umoja wa Mataifa vilivyowekewa kaskazini baada ya majaribio yake ya tatu ya nyuklia mwezi Februari.

Mazishi ya Chinua Achebe yaanza

Mazishi ya mwandishi maarufu wa riwaya wa Nigeria, Chinua Achebe, yameanza katika mji wa Ogidi, kusini-mashariki mwa nchi ambako ndiko alikotoka.
Chinua Achebe
Maziko yanaendelea kwa juma zima, kumkumbuka na kusherehekea maisha ya mmoja kati ya waandishi maarufu kabisa wa Afrika.
Bwana Achebe alifariki mwezi March akiwa na umri wa miaka 82.
Kongamano la waandishi, mihadhara ya wasomi na kanivali ni baadhi ya matukio katika mazishi ya wiki moja ya mwandishi Chinua Achebe.
Shughuli zitakuwa nyingi katika mji wa Ogidi alikozaliwa kusini-mashariki mwa Nigeria.
Wageni kutoka pembe zote za dunia wanatarajiwa kutoa heshima zao za mwisho kwa yule waliyemwita baba wa fasihi ya kisasa ya Afrika.
Bwana Achebe aliwakosoa viongozi wa Nigeria, hata hivo wanasiasa wengi maarufu wanatarajiwa kuhudhuria matanga yake.
Maziko yatafuata taratibu za Kikristo na utamaduni wa kabila lake la Igbo.
Chinua Achebe alikuwa maarufu kwa mtindo wake wa uandishi ambao umefuata mila ya kutoa hadithi ya kabila lake la Igbo.
Kitabu cha Chinua Achebe Things Fall Apart kimetafsiriwa katika lugha zaidi ya 50.

Friday 17 May 2013

Maafisa wa usalama wa Misri watekwa nyara Sinai


Maafisa saba wa usalama wa Misri, wametekwa nyara na watu wasiojulikana katika Rasi ya Sinai , kwa mujibu wa maafisa wa Misri. Maafisa hao , Polisi watatu na wanajeshi wanne walitekwa wakati wakisafiri katika basi dogo Kaskazini mwa Sinai mashariki mwa mji wa El Arish.
Watekaji nyara wanasemekana kudai kuachiliwa kwa jamaa zao wanaozuiliwa katika gereza la Misri
Ripoti zinaarifu kuwa viongozi wa kikabila wa Bedouin, wametakiwa kuingilia kati.
Rais Mohammed Morsi amewaita waziri wake wa ulinzi na waziri wa mambo ya ndani kwa mkutano wa dharura baada ya kutekwa nyara kwa maafisa hao.
Maafisa wanasema watu waliokuwa wamefunika nyuso zao waliteka teksi mbili nje ya mji wa el-Arish, na kuwakamata polisi na askari kisha wakarejea mjini Cairo.
Matukio mengi ya uhalifu yamekuwa yakiongezeka katika Kanda hiyo tangu alipong’olewa mamlakani rais Hosni Mubarak mwaka 2011.
Wanamgambo wa kiislam wamekuwa wakitumia eneo hilo kama ngome ya mashambulio dhidi ya vikosi vya usalama vya Misri na Israeli
Rasi ya Sinai imekuwa eneo lenye visa vingi vya uhalifu tangu rais Hosni Mubarak kung’olewa mamlakani mwaka 2011.
Kumekuwa na matukio kadhaa ambapo watalii kutoka nchi za kigeni wametekwa nyara katika eneo hilo.
Duru zinasema kuwa kawaida wao huachiliwa haraka lakini wahamiaji wengine kutoka nchi maskini wanaokwenda huko kutafuta maisha mazuri, wamewahi kutekwa nyara na kuteswa vibaya na watu wanaofanya biashara haramu ya binadamu eneo la Sinai

Askofu Mtega afafanua sababu za kustaafu kwake

Askofu Mkuu Mstaafu wa jimbo Katoliki la Songea, Mhashamu Norbert Mtega
Askofu Mkuu Mstaafu wa jimbo Katoliki la Songea, Mhashamu Norbert Mtega
Askofu Mkuu Mstaafu wa jimbo Katoliki la Songea Mhashamu Norbert Mtega ametoa ufafanuzi juu ya uamuzi wake wa kumuomba Baba Mtakatifu kustaafu na kusema amefanya hivyo kwa maslai ya jimbo kuu Katoliki la Songea baada ya kubaini kuwa afya yake haimwezeshi kumudu majukumu ya kiutawala ya jimbo hilo.
 Askofu Mtega mwenye umri wa miaka 68 amesema licha ya kustaafu kwake ataendelea kufanya majukumu ya kitume kama kawaida na amechagua kuishi Songea baada ya kustaafu huku akitaka wakatoliki wa jimbo hilo wasiwe na wasiwasi na uamuzi wake.
Baada ya saa kadhaa za maombi ya wandishi wa habari waliokua na kiu ya kuzungumza na Askofu huyo juu ya uamuzi wake wa kuomba kustaafu na hatimaye kukubaliwa na Baba Mtakatifu Papa Francis, hatimaye wakakutana nae majira ya jioni, na kwanza ilikua ni kutaka ufafanuzi wa kwa nini amechukua hatua hiyo iliyoshitua watu wengi.
Pili, waandishi wa Habari walitaka kujua kwa nini afanye hivyo wakati umri wake wa kustaafu kwa hiari ambao ni miaka 70 haujafika, wala kustaafu kwa lazima ambao ni miaka 75 hajafikia na tatu, tukataka kujua Askofu Mtega angependa Askofu Ajae afanye nini kwa maslai ya jimbo kuu katoliki la Songea.
Aidha Askofu Mtega amesema hakuna lolote baya lililosababisha yeye astaafu kazi hiyo ya kuhudumia jimbo kuu katoliki la Songea ambalo kiutawala linasimamia majimbo nane ya kusini mwa Tanzania.
Gerson Msigwa, TBC Ruvuma.

Wapenzi wa jinsia moja wabaguliwa Ulaya


Wapenzi wa jinsia moja huhofia kuripoti kwa polisi visa vya dhulma dhidi yao
Muungano wa Ulaya umetoa ripoti kuonyesha kuwa zaidi ya robo ya wapenzi wa jinsia moja waliohojiwa wameshambuliwa ama kutishwa katika miaka mitano iliyopita.
Ripoti hiyo iliandaliwa na wataalamu wa muungano huo kuboresha sera zinazoelekea kutenga watu kutokana na hulka zao za mapenzi.
Watu elfu tisini na tatu wanaoishi Ulaya walihojiwa kuhusu namna wapenzi wa jinsia moja wanavyochukiwa na kutengwa. Majibu yao yaliyowasilishwa kwenye mtandao yalionyesha katika miaka mitano zaidi ya robo walishambuliwa ama kutishwa.
Na shuleni wanafunzi wawili kati ya watatu waliohojiwa walisema kuwa walificha kuwa wao ni wapenzi wa jinsia moja.
Kinachotia wasiwasi ni kuwa zaidi ya nusu yao hawako radhi kuripoti visa vya kushambuliwa kwa polisi kwa sababu wanaamini kuwa hakuna kitakachofanyika.
Wanasiasa na watunga sera mia tatu wanakutana Hague Uholanzi kujadili njia mpya za kuwalinda watu na kuhakikisha kuwa hawashambuliwi hata wakipendelea mapenzi ya jinsia moja.

Thursday 16 May 2013

MPANDA FM MATUKIO 16/05/2013



Mbeya
Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Lupata, inayomilikiwa na Jumuiya ya Wazazi (CCM) wilayani Rungwe wamefanya vurugu na kuliteketeza kwa moto bweni la wavulana wakipinga kitendo cha wanafunzi wenzao watatu kusimamishwa masomo kwa utovu wa nidhamu.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, Diwani Athuman, amesema vurugu hizo zilitokea juzi majira ya saa 2:00 usiku baada ya wanafunzi waliosimamishwa masomo kuwahamasisha wenzao kupinga adhabu hiyo.
Kamanda Diwani amesema tukio hilo limesababisha uharibifu mkubwa wa mali za shule hiyo ingawa moto huo haukusababisha madhara.
Amesema chanzo cha vurugu hizo ni kutokana na wafunzi hao; Joseph Robert (18) mwanafunzi wa kidato cha nne, Mwita Chacha (17) mwanafunzi wa kidato cha tatu wote wakazi wa Kitunda, Dar es Salaam kusimamishwa masomo kwa utovu wa nidhamu.
Amesema mwanafunzi mwingine anayehusika katika kuhamasisha wenzao kufanya vurugu hizo ni Daniel David (18) anayesoma kidato cha tatu na mkazi wa Ipinda, wilayani Kyela.
Kutokana na tukio hilo, amesema wanafunzi 15 wakiwamo waliosimamishwa masomo wanashikiliwa na polisi kwa ajili ya mahojiano zaidi.


Arusha
Wadau wa utalii kutoka halimashauri ya Wilaya ya longido wamekutana mjini arusha katika mkutano wa Siku Mbili wenye lengo kuu la kutathimini na kutambua mchango wa Rasilamali zinazo wazunguka wafugaji wa haliamashauri hiyo katika kujiletea uchumi kwa njia nyingine tofauti na ile iliyozoeleka

Mkutano huo wa Wadau hao wa Utalii kutokandani ya Halimashauri ya Wilaya ya longido ambao ulifunguliwa na Afisa wa Mazingira ya Ikolojia kutokea  mamlaka ya Hifadhi za Taifa Bwana  Alibert Mziray ambapo amesema kuwa kuna umuhimu mkubwa  wa kujua jinsi ya kutumia Rasilimali zilizopo  hasa kwa Wafugaji hao wa Loliondo.

Amesema kuwa jamii hizo zinatakiwa kutambua kuwa kuna umuhimu mkubwa  wa kutambua kuwa mazingira ya asili yaliyowazunguka wafugaji wa kiasili yana umuhimu mkubwa na ushirikiano nao hivyo inabidi wangalie jinsi gani watashirikiana na mazingira yao katika maisha yao ya kila siku.

pamoja na hayo mkutano huo uliwakuatanisha wadau hao wa utalii unatarajia kujadili na kupata njia muafaka za kumsaidia mfugaji wa kiasili katika kufanya ufugajiwake uwe na tija ya kiuchumi sambamba na kuwafanya wafugaji hao kutotegemea mifugo na kuangalia njia nyingine za kiuchumi zitakazo wafanya wapate maendeleo.

Kwa sasa hivi mradi wa BFFS wilayani longido wamefanikiwa kuwafikia zaidi ya wamasai 300 ambapo zaidi ya asiliamia 90 ni wanawke ambapo wamefanikiwa kwa awmu ya kwanza kuwapatia mkopo wa zaidi ya milioni 90 kwa vikundi zaidi ya 30 ambapo wamelenga kwa awamu ya pili kuvipatia vikundi vipatavyo 48 mkopo wa kuwasaidi kaya hizo za wafugaji.


 Arusha 16/05/2013

MKE wa waziri mkuu Mama Tunu Pinda amewaasa Makatibu Muhtasi na kuwataka wazingatie maadili ya taaluma yao ya uhazili ili kuongeza ufanisi wa majukumu ya kazi zao.

Ametoa wito hu o leo  wakati akifungu Kongamano la Tatu la Makatibu Muhtasi (Tanzania Personal Secretaries Association – TAPSEA) kwenye ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa Arusha (AICC), Jijini Arusha.

Kongamano hilo la siku mbili, limehudhuriwa na Makatibu Muhtasi zaidi ya 1,500 kutoka mikoa yote nchini, na baadhi ya wawezeshaji kutoka Kenya, Uganda na Rwanda.

Amewataka waongeze jitihada za kukimarisha Chama cheo ili hatimaye TAPSEA iweze kuenea Mikoa yote na kuwa Chombo kitakachosimamia miiko na maadili ya fani ya Uhazili.

Amesema majukumu ya makatibu muhtasi siyo kupiga chapa pekee na kuongeza kwamba, kama chama cha kitaaluma, TAPSEA lazima iendeleze jitihada za kubadili mtazamo huo ili jamii iweze kutambua umuhimu wa nafasi ya makatibu muhtasi katika taasisi mbalimbali za umma na za sekta binafsi.


Mama Tunu Pinda amesema kuwekeza katika teknolojia ni jambo muhimu lakini teknolojia pekee haiwezi kuleta mabadiliko chanya katika kuboresha huduma na kuongeza tija

Mama Tunu Pinda pia amezindua TAPSEA SACCOS na kuwataka makatibu muhtasi hao wajiunge kwa wingi ili kutunisha mfuko wa chama chao.

Mapema, akimkaribisha kuzungumza na washiriki wa mkutano, Mlezi wa TAPSEA Dk. Mary Nagu ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Uwekezaji na Uwezeshaji aliwataka wawe waaminifu katika kuijenga TAPSEA SACCOS ili hatimaye ifikie hatua ya kuwa benki yao maalum kama ilivyo kwa Chama cha Walimu nchini.

Naye Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Bi. Angela Kairuki ambaye pia mshauri wa Kisheria wa TAPSEA aliwataka washiriki wa kongamano hilo kuzingatia maadili kwa kutunza siri za ofisi wanazozitumikia.

 

 Arusha 16
Jeshi la Polisi mkoani Arusha limekanusha taarifa ya kuachiwa huru kwa mtuhumiwa wa ujangili  Bw. Frank William Silangei maarufu kwa jina la “Ojung’s Mwarusha” mkazi wa Ngaramtoni Kibaoni.
Fatma amasi
Kamanda wa polisi mkoa wa Arusha Liberatus Sabas amesema kuwa mtuhumiwa huyo mwenye umri wa miaka 32  hivi sasa yuko mahabusu na taratibu za kumfikisha  mahakamani zinaendelea kufanyika.
Kamanda Sabas ameeleza kuwa  mtuhumiwa  Silangei hajaachiwa huru kama ilivyoripotiwa
Kamanda Liberatus Sabas amesema Serikali kupitia Jeshi la  Polisi  itaendelea na jitihada zake za kuhakikisha kuwa vitendo vyote vya ujangili vinatokomezwa na yeyote atakayehusika na vitendo hivyo atachukuliwa hatua za kisheria.


  
 Wakurugenzi wa Upelelezi wa makosa ya jinai kutoka nchi 25 barani Afrika wametakiwa kutumia vizuri mafunzo ya Operesheni za pamoja ili kuweza kukabiliana na uhalifu ikiwemo vitendo vya ugaidi na uhamiaji haramu vinavyojitokeza katika nchi za Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika kwa kasi hivi sasa.

Aziza seif
 Hayo yamesemwa  na  Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Nchini DCI Robert Manumba wakati akizungumza na waandishi wa habari baada ya kufungua Mafunzo kwa Wakurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai kutoka Umoja wa Wakuu wa Polisi Kusini mwa Afrika (SARPCCO) Pamoja na Umoja wa Wakuu wa Polisi Afrika Mashariki  (EAPCCO) kuhusu kufanya operesheni za pamoja kukabiliana  na uhalifu unaovuka mipaka.

 DCI Manumba amesema uhalifu unaofanyika hapa nchini na ukanda huu wa Afrika Mashariki ndio huo huo unaotokea katika nchi nyingine hivyo ushirikiano na kubadilishana taarifa kutasaidia kutambua na kuweka mikakati thabiti ya kuweza kudumisha amani na usalama katika bara la Afrika.


Kwa upande wake Mkuu wa Polisi wa Kimataifa INTEPOL kanda ya Afrika Mashariki kutoka Nchini Kenya Bw.Rego Francis amesema Majeshi ya Polisi yana wajibu wa kutoa  elimu ya kutosha kwa wananchi ili waweze kutoa taarifa za uhalifu mapema kwa vyombo vya usalama ili ziweze kufanyiwa kazi mapema kabla ya matukio kutokea.

 Naye Mkuu wa Kitengo cha Polisi wa Kimataifa (INTEPOL) Tanzania    Kamishna Msaidizi wa Polisi Gustavus Babile amesema Mafunzo hayo ya siku mbili lengo lake ni kubadilishana uzoefu na kupeana mbinu na kuweka mikakati ya kufanya operesheni  zitakazoweza kuutokemeza uhalifu.

 Babile amesema kupitia mafunzo hayo wataweza kuandaa Operesheni zenye mafanikio zitakazoweza kushirikisha nchi nyingi katika kukabiliana na Ugaidi, Madawa ya kulevya, wahamiaji haramu, wizi wa magari na uhalifu wa aina nyingine unaotokea hapa Afrika.

Mafunzo hayo yanafanyika baada ya kumalizika kwa Mkutano wa kumi na nane wa Wakuu wa Polisi kusini mwa Afrika  ambapo katika maazimio yaliyofikiwa ni pamoja na kufanya operesheni za pamoja baina ya SARPCCO na EAPCCO.