Thursday 7 November 2013

JINI KABULA ANYWA SUMU KISA PENZI LA CHUZ...

  Nyota wa Tamthiliya ya Jumba la Dhahabu, Miriam Nyafulwa Jolwa ‘Jini Kabula’ aliwahi kunywa sumu ambayo haikujulikana mara moja huku chanzo kikiwa ni ugomvi wa kimapenzi na mzazi mwenzake, Tuesday Kihangala ‘Chuz’. Akizungumza na mwandishi wetu mwanzoni mwa wiki hii, Chuz alisema tukio hilo lilijiri mwaka 2011 nyumbani kwake, Makongo jijini Dar na kwamba  siku hiyo hataisahau kutokana na jinsi alivyochanganyikiwa na hali ilivyokuwa. Aidha, Chuz alisema walikuwa na ugomvi mdogo tu wa kimapenzi jambo ambalo alitarajia kuwa lingeisha kwa amani. Lakini tofauti na matarajio yake, kila dakika iliyokuwa ikiondoka Kabula alizidi kupandisha mori kama si maruhani. Alisema muda mfupi baadaye, Jini Kabula  alivunja vioo vya gari lake kwa kutumia mawe kitendo kilichompa sababu Chuz kumpeleka polisi (hakutaja jina la kituo). Hata hivyo, Chuz aliendelea kushusha ‘vesi’ kuwa baada ya siku mbili, Jini Kabula alitolewa kwa dhamana huku yeye  akidhani kuwa yameisha lakini Kabula aliendeleza ‘libeneke’ ambapo alifika nyumbani  kwake na kujifungia ndani kisha akanywa dawa ambazo zilidaiwa kuwa ni sumu kali. “Nilipokuta mlango umefungwa nilianza kubisha hodi bila mafanikio. Niliamua kwenda polisi, wakaja na kuvunja mlango na kumkuta akiwa amelala chali huku akiwa anatokwa na povu jingi kinywani,” alisema Chuz.
Baadaye walimpa huduma ya kwanza kabla ya kumkimbiza hospitali (jina tunalo) kwa matibabu zaidi. Hata hivyo, baada ya kutibiwa, Chuz aliomba yaishe kwa amani.
“Kaka sitaisahau siku hiyo, ilikuwa  mbaya sana kwangu. Jini Kabula alikuwa kabadilika kabisa, alidhamiria kujiua kweli. “Nashukuru hamkupata habari hiyo lakini ilinichanganya sana,” alisema Chuz.
Mwandishi alimtafuta Jini Kabula kwa njia ya simu ili kuthibitisha juu ya habari hizo ambapo baada ya kusomewa madai hayo alianza kwa kucheka na kujibu:
“Duh! Wewe ni kiboko, umezipata wapi hizo habari? Lakini sipendi kuzungumzia mambo ya zamani, muulize vizuri aliyekwambia.”

No comments:

Post a Comment