Thursday 24 October 2013

Wema Sepetu atumia milioni 13 kuibadili ngozi yake akiwa China baada ya kuharibiwa sana na Mkorogo


IMEVUJA! Kumbe ile safari ya nchini China ya Miss Tanzania 2006, Wema Sepetu ‘Madam’ lengo lilikuwa kubadili ngozi ya mwili wake katika mwonekano mpya ambayo ilishaharibika kwa mkorogo.
 
Wema Sepetu ‘Madam’.
 
Kwa mujibu wa chanzo chetu makini, staa huyo aliingia nchini humo na mdogo wake aitwaye Bite ambaye kazi yake kubwa ilikuwa kufanya mawasiliano na nyumbani, Tanzania endapo lingetokea baya wakati wa zoezi hilo.
 

KWA NINI ALIAMUA KUDILI NA NGOZI?
Mpashaji wetu aliliambia Amani kwamba, Wema alichoshwa na ‘vijembe’ vya watu mbalimbali wakiwemo wabaya wake kuwa ngozi yake imebabuka kwa kutumia mkorogo kupitiliza.
 
Miguu ya Wema Sepetu ‘Madam’ kabla ya kubadili ngozi.
 
“Kuna wakati Wema alikuwa akikosa amani kutokana na maneno ya watu, wengine waliokuwa wakimrushia vijembe ni masupastaa wenzake, ndiyo maana akaamua kwenda China kubadili ngozi yake iwe na mwonekano mpya,” kilisema chanzo.

Habari zaidi zilidai kwamba, supastaa huyo hakupenda kabisa Wabongo wajue kuwa yupo China kubadili ngozi, hata baadhi ya magazeti yalipoandika amekwenda kujirusha na msanii wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond’ alimshukuru Mungu siri yake imesitirika.

UBADILISHAJI WA NGOZI WATUMIA SAA 12
Kwa mujibu wa chanzo chetu, Wema aliingia kwenye kliniki ya ngozi katikati ya mwezi Oktoba, saa 3:12 asubuhi na shughuli ikamalizika saa 2:25 usiku.
 
“Alikaa kliniki toka saa tatu na dakika kumi na mbili asubuhi hadi saa mbili na dakika ishirini na tano usiku,” kilisema chanzo.
 
MADAKTARI WAMWONYA
Habari zaidi zinaeleza kuwa, madaktari waliokuwa wakimfanyia zoezi hilo walipomaliza walimuonya kutorudia tena kutumia mikorogo au aina yoyote ya losheni zenye kubabua ngozi, kama vile carolite.
 
SEHEMU ZILIZOHARIBIKA SANA
Kwenye mwili wa Wema, sehemu zenye mikunjo kama nyuma ya magoti, kukaribia makwapa, mapajani na mbele ya viwiko ndizo ziliongoza kwa kuharibika hali iliyokuwa ikimfanya mara nyingi ashindwe kuvaa sketi za vimini.
 

SHILINGI MILIONI 13 ZAYEYUKA
Katika zoezi hilo, Wema ambaye pia ni msanii wa filamu za Bongo na bosi wa Kampuni ya Filamu ya Endless Fame Production ya jijini Dar, ametumia shilingi za Tanzania, milioni 13 ikiwa ni pamoja na nauli yake na Bite kwenda China na kurudi, malazi na chakula.
 
APEWA DAWA YA KUZUIA KUZEEKA MAPEMA
Baada ya ubadilishaji huo wa ngozi, Wema alipewa dawa ambazo zitamsaidia kutozeeka mapema.
 
AONYWA MATUMIZI YA SIGARA NA KUTOLALA KWA WAKATI
Mbali na dawa hizo, staa huyo alionywa na matumizi ya sigara aina yoyote ile na kujipanga upya kwenye suala la kulala mapema ili apate usingizi wa kutosha.
 

MENEJA WAKE ATINGA CHINA KUHAKIKI NGOZI
Habari zaidi zikawekwa wazi kwamba, Wema alimwita meneja wake, Martin Kadinda kwa lengo la kuhakiki mwonekano mpya wa ngozi ya staa huyo.
 
Juzi, Amani lilimtafuta Dk. George wa zahanati maarufu ya Sino iliyopo Sinza Mapambano (Kwawachina) ambapo alisema warembo wengi hubadili ngozi kwa mtindo wa plastic surgery, mara nyingi sehemu yenye mikunjo au kuharibika hukatwa na kuvutwa, kama mtu alishaanza kuzeeka huonekana kijana.
 
“Nchi maarufu kwa kubadili ngozi ni Thailand, lakini China na Afrika Kusini zimeanza  kutoa huduma hiyo.
 
“Hapa nchini bingwa wa masuala ya ngozi ni Profesa Masawe, zamani alikuwa Muhimbili kwa sasa ana kituo chake upanga Dar,” alisema Dk. George.
 
Kuhusu madhara, Dk. George alisema hayako wazi sana inategemea maisha ya mtu ya kila sikiu.

MENEJA WA WEMA AZUNGUMZA
Baada ya gazeti hili kuzinyaka habari hizo, lilimtafuta meneja wa Wema, Martin Kadinda alipoulizwa alikiri kwenda China kwa ajili ya kuhakiki mwonekano mpya wa ngozi ya ‘Beautiful Onyinye’ huyo na kusema kuwa ilikuwa lazima bosi wake afanyiwe hivyo kwa sababu bosi ni kioo cha jamii.
 
“Unajua Wema ni kioo cha jamii, hivyo si vyema watu kumsema kwa kitu kidogo kuhusu ngozi yake kwani hata yeye alikuwa hapendezwi nayo. Lakini nashukuru sana kwa sasa ana mwonekano mpya wa ngozi.

“Nilikwenda kuhakikisha kama ngozi yake kwa sasa inaweza kuwa na mwonekano mpya, ni kweli wamefanikiwa madaktari. Wamempa masharti kadhaa, kama kulala sana,  lakini pia wamempa dawa nyingine,” alisema Kadinda.
 

WEMA MWENYEWE SASA
Baada ya kuzungumza na Kadinda, Amani lilimuendea hewani Wema ili kumsikia na yeye kuhusu kubadili ngozi nchini China.

Amani: Mambo Wema, za China?
Wema: Salama tu, niambie.
 
Amani: Hapa kuna habari kuwa safari yako ya China ilikuwa kwa ajili ya matengenezo ya ngozi yako, vipi ni habari za kweli?
Wema: Ah! Sasa ngozi yangu imekuaje kwani?

Amani: Inasemekana una mwonekako mpya wa ngozi, ile ya kwanza hukuipenda kwa sababu ya kujeruhiwa na mkorogo.
Wema: (kimya kidogo) oke, sikupenda kulizungumzia hilo kwa sasa lakini ndiyo hivyo kama ulivyosikia.

Amani: Unaweza kuniambia ni shilingi ngapi umetumia?
Wema: Mh! Mbona unanikaba koo jamani? Kama shilingi 
milioni 13 pamoja na gharama za usafiri.

Amani: Nashukuru sana Wema.
Wema: Karibu sana.

Chanzo: Gazeti la Amani, toleo la leo

No comments:

Post a Comment