Sunday 22 September 2013

Qatar yawatoa wasiwasi kuhusu Kombe la Dunia 2022



Qatar imesisitiza kuwa inaweza kuandaa dimba la Kombe la Dunia mwaka wa 2022 katika majira ya joto, hata wakati Shirikisho la FIFA likiendelea kuwekewa mbinyo wa kuhamisha tamasha hilo hadi msimu wa baridi 

Taifa hilo lenye utajiri wa nishati, ambako nyuzijoto hufikia sentigredi 45 ilipewa kibali cha kuandaa Kombe la Dunia miaka mitatu iliyopita katika uamuzi wa kushangaza.
Qatar inasema inaweza kukubali kuhamisha dimba hilo hadi msimu wa baridi lakini ikasisitiza kuwa licha ya joto kali, inaweza kuandaa Dimba la Dunia msimu wa joto kwa kujenga viwanja vyenye hewa ya baridi kwa kutumia teknolojia mpya inayojali mazingira.
Namna ambavyo mashabiki wataweza kukabiliana na joto, nje ya viwanja, bado ni suala linalotia wasiwasi na Rais wa FIFA Sepp Blatter hivi karibuni amesema lilikuwa kosa kupanga kinyang'anyiro hicho cha msimu wa joto, katika taifa la jangwa.
Rais wa Shirikisho la Soka barani Ulaya UEFA, Michel Platini pia amethibitisha kuwa mashirikisho 54 wanachama wa UEFA wamekubaliana kwa kauli moja kuhusu wazo la kuhamisha dimba hilo la Qatar, hadi msimu mwingine wa mwaka
Lakini nayo kamati andalizi ya Qatar imejaribu kuondoa wasiwasi hiyo, kwa kusema teknolojia ya kuleta hewa ya baridi, kwa kutumia solar, katika maeneo ya umma, nje na ndani ya viwanja, huenda ikatatua shida hizo.
 



No comments:

Post a Comment