Shirikisho la soka ulimwenguni FIFA limetishia kutimua Nigeria kutoka kwa shirikisho hilo iwapo Chris Giwa hataacha kujidai kuwa rais wa shirikisho la soka nchini humo.
Shirikisho hilo limesema Nigeria ina hadi Jumatatu kubadili mambo kwani halimtambui bwana Giwa kama Rais wa shirikisho la soka nchini humo.
Ikiwa shirikisho hilo litawekewa marufuku, marufuku hiyo itaondolewa tu iwapo bodi halali iliyoishidhishwa kushika uongozi , Aminu Maigari akiwa rais wake, itaruhusiwa kuendelea na kazi zake.
Uchaguzi mpya utahitajika kufanywa haraka iwezekanavyo.
Siku ya mwisho kwa Giwa kujiondoa kama rais wa NFF ilifikiwa na FIFA Jumatano. Hii ni baada ya Giwa kukosa kutii makataa ya kuondoka ofisini iliyowekwa na Fifa ya tarehe 1 Septemba.
Iwapo Jumatatu itafika na Giwa hatakuwa amejiondoa kama Rais,basi Nigeria ambao ni mabingwa Afrika hawatashiriki michunao ya kufuzu kwa mechi za kombe la taifa bingwa Afrika itakayochezwa Afrika Kusini Septemba 10.
Hata hivyo shirikisho la soka Afrika limesema kwamba ikiwa Super Eagles watakosa mechi ya kufuzu, basi watatimuliwa kutoka kwa mashindano ya kufuzu kwa kombe hilo.
Nigeria ilipigwa marufuku kutocheza soka ya kimataifa kwa siku tisa mwezi Julai sababu kuu ikiwa serikali kuingilia usimamizi wa soka baada ya Magairi kuondolewa kama Rais wa shirikisho la soka nchini humo kufuatia uamuzi wa mahakama.
Kamati ya usimamizi wa NFF ilimuondoa Maigari uongozini kwa kura siku chache tu baada ya mahakama kuamua vinginevyo. Hata hivyo FIFA haikukubali kitendo hicho na hapo ndipo Magariri alirejeshewa wadhifa wake tena mwezi Agosti.