Sunday 7 September 2014

RIO FERDINAND: MANCHESTER UNITED WENDAWAZIMU KUMUUZA WELBECK KWA ARSENAL


    BEKI wa zamani wa Manchester United Rio Ferdinand ameonyesha mshangao wake kwa kocha Louis van Gaal kumuuza mshambuliaji Danny Welbeck kwa washindani wao wakubwa – Arsenal.

    Welbeck aliyeibuliwa kutoka academy ya Manchester United, amesajiliwa Emirates kwa pauni milioni 16 katika siku ya mwisho ya dirisha la usajili la kiangazi.
    Rio ambaye kwa sasa anakipiga na QPR, amehoji maamuzi hayo ya Van Gaal kumuuza Welbeck – ambaye anadhani alikosa furaha dhidi ya Robin van Persie na Wayne Rooney ambao siku zote wamekuwa mbele yake katika kikosi cha kwanza.
    Akiongea na The Sun on Sunday Rio akasema: “Siamini kuwa United wamemuuza Welbeck, haswa kwa Arsenal. Kwangu mimi naona kama ni uwendawazimu.
    “Alikuwa tishio kwa mabeki na kama Arsenal watamtumia vizuri atakuwa hatari sana kwao.
    “Nadhani alichanganyikiwa na namna alivyokuwa anachukuliwa na United, kwa sababu hata alipokuwa anafanya vizuri bado Rooney na Van Persie wanakuwa chaguo la kwanza. Nitashangaa kama watajutia kumuuza”.
    Mchezo unaofuata wa Ferdinand kwa QPR ni dhidi ya United ambapo atakutana na timu hiyo kwa mara ya kwanza tangu alipohitimisha miaka yake 12 Old Trafford.

    No comments:

    Post a Comment