Monday 22 September 2014

Waziri Mkuu alitetea Bunge la Katiba, asema yuko radhi ifanyike Kura kuhusu Muungano



Waziri Mkuu Mizengo Pinda amesema mchakato wa Bunge la Katiba unaoendelea hivi sasa ni halali na wa kisheria.
Ametoa kauli hiyo jana wakati akizungumza na waumini na viongozi mbalimbali waliohudhuria ibada ya uzinduzi wa dayosisi mpya ya Ziwa Tanganyika ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) na kuwekwa wakfu kwa Askofu Ambele Anyigulile Mwaipopo aliyeteuliwa kuongoza dayosisi hiyo.
Waziri Mkuu alikuwa akitoa ufafanuzi wa hoja ya Askofu Mwaipopo aliyetaka maoni ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba yaheshimiwe,  na Bunge Maalum la Katiba lisitishwe kama ambavyo Jukwaa la Katiba limetaka na pia tamko la Jumuiya za Kikristo Tanzania (CCT)
Waziri Mkuu amesema Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na Tume hiyo siyo Katiba bali ni mawazo yaliyokusanywa ambayo yanapaswa kupitiwa na chombo kingine cha kisheria ambacho ni Bunge Maalum la Katiba.
Amesema muda ambao Tume hiyo ilipewa haukuwa mrefu sana kwa hiyo isingekuwa rahisi kwa wajumbe wake kuzingatia kila eneo linalogusa maisha ya Watanzania.
Mh. Pinda amesema  kinachowachanganya Watanzania ni suala la Serikali mbili au tatu lakini katika makabrasha ya Tume ambayo wajumbe wote walipewa, suala la Muungano halikupewa kipaumbele na Watanzania wengi waliotoa maoni yao.
Ameongeza kuwa  kwa mujibu wa takwimu za Tume ya mabadiliko ya katiba  watu waliotaka Muungano wa Serikali tatu ni kati ya asilimia 12 na 13 hivyo  Haiwezekani  takwimu hizo zitajwe kama matakwa  ya Watanzania wengi.”
Waziri Mkuu amesema yuko radhi ifanyike kura mahsusi ya kuwaomba Watanzania waseme kama wanataka Muungano na tena uwe ni wa aina gani.
Aidha Amewasihi Maaskofu, wachungaji na viongozi wengine wa dini waliohudhuria uzinduzi huo waendelee kuuombea mchakato huo wa katiba  ili uishe vizuri.  
Katika hatua nyingine bunge maalum la katiba limeahirisha shughuli ya uwasilishaji wa rasimu uliokuwa ufanyike leo bungeni mjini Dodoma, ili kutoa muda kwa kamati ya uandishi kukamilisha shughuli hiyo na kuwasilisha keshokutwa Jumatano.

No comments:

Post a Comment