Saturday 6 September 2014

JUHUDI ZAIDI ZAHITAJIKA KUPUNGUZA WATU KUJIUA DUNIANI- WHO



Shirika la Afya Duniani, WHO, limetoa wito hatua mathubuti zichukuliwe ili kupunguza visa vya watu kujiua duniani, huku idadi ya watu wapatao zaidi ya 800,000 wakiwa wanajiua kila mwaka.

WHO imesema kuwa ni nchi 28 tu zinazojulikana kuwa na mikakati ya kuzuia watu kujiua. Katika ripoti yake ya kwanza ya kimataifa, WHO imesema kupunguza upatikanaji wa vifaa vya kujiua kama vile bunduki na dawa za kuuwa kwekwe na wadudu, pamoja na kuboresha upatikanaji wa huduma za afya ya akili ni muhimu katika kuzuia watu kujiua.
 
Ripoti hiyo pia inatoa wito kuwepo uwajibikaji katika kuripoti visa vya kujiua katika vyombo vya habari, kwa kuepukana na matumizi ya maneno ya uchochezi na kueleza kwa kina njia zinazotumiwa.
Dkt. Shekhar Saxena ni mkurugenzi wa idara ya afya ya akili na matumizi mabaya ya dawa katika WHO:
 
"Kujiua hutokea aghalabu miongoni mwa watu wenye umri wa miaka zaidi ya 50, lakini pia ni sababu kubwa ya vifo miongoni mwa vijana. Ni sababu ya pili ya vifo miongoni mwa vijana kati ya umri wa miaka 15-29. Kwa ujumla duniani, wanaume wengi zaidi hujiua kuliko wanawake. Hata hivyo, ujumbe katika ripoti hii unahusu zaidi kile inachokiamini WHO kuwa kujiua kunaweza kuzuiliwa."
 
WHO pia inatoa wito uhalifishaji wa kujiua uondolewe, ikizingatia kuwa kuwafunga watu waliojaribu kujiua siyo njia mwafaka ya kuzuia kujiua.

No comments:

Post a Comment